1985 - 2007


5. Mtindo wa Maisha wa Mwinjilisti
Je, ni kitu gani kinachowafanya watu wasikilize?

Support Pages   Index To All Lessons   School of Finances  
World Christian News   
Who Are We?   Site Index


Katika Biblia Yako Soma
Marko 1

Mstari wa Kukariri
(Yesu) akasema, "Wakati umetimia, na Ufalme wa Mungu umekaribia; tubuni, na kuiamini Injili” (Mk 1:15).

Baadaye Zungumzieni Jambo Hili
Peaneni changamoto kwa kuulizana maswali yaliyoko mwishoni mwa somo

Jambo la Kufanya Kabla Hatujakutana Tena
Ni wakati wa kutenda yale Yesu aliyotenda, kwa kwenda katika kijiji ambacho hujawahi kufika na kuhubiri huko. Baada ya maombi nendeni wawiliwawili, au kama kikundi kwa pamoja.

Kazi ya Kuandika Ya Stashahada
Pitia vitabu vya Injili na Waebrania 5:7 kisha andika ukurasa mmoja ukielezea maisha ya Yesu kimaombi.

Tafakari Mistari Hii Neno Kwa Neno
Waebrania 2:3,4

Tumia Dakika Moja Kuubadilisha Ulimwengu
Ombea taifa la Mongolia
Idadi ya watu: 3,000,000
Waamini wanaweza kuwa ni 1,000 tu
Kuna mateso mengi na unyonyaji

 

 

Hakikisha umewafundisha wengine somo hili.
Kila mara omba na kujiandaa ukiongezea mistari mingine ya Biblia
na mifano yako mwenyewe ili kufanya somo lieleweke vizuri zaidi.
 


Marko 1:45 inatuambia kwamba watu walikuja kwa Yesu kutoka kila mahali. Watu hao hawakuja kanisani, wala kwenye mikutano ya Injili, wala kwenye umisheni au kazi nyingine. Walikuja kwa Yesu. Kama tukiweza kugundua ni kwa nini walikuja, na tukafanya kama alivyofanya Yesu, watu wataendelea kuja kwa Yesu hata sasa kutoka pande zote.

1. Yesu Alimkaribisha Roho Mtakatifu

Yesu alimsikiliza Roho Mtakatifu, (Mk 1:9-12), alitii na kujiachia Yeye na huduma yake kwa uongozi wa Roho, akienda na kutenda sawasawa na maelekezo ya Roho.

Kwanini Jambo Hili Ni Muhimu Kiasi Hicho?
Yesu alikuwa, na hata sasa ni Mungu, lakini alipozaliwa aliamua kuacha uweza wake wa kimbingu (Flp 2:6,7). Alichagua kuja kama mtoto mchanga wa kawaida ya kibinadamu, na sio kama jemadari, au mfanyabiashara tajiri, au mtawala mwanasiasa. Yesu aliishi kama mwanadamu wa kawaida; na kama sisi alihisi baridi, njaa, kiu, furaha na huzuni. Alihudumu pia kama mwanadamu wa kawaida, lakini kama mwanadamu aliyepewa uweza na Roho Mtakatifu. Vivyo hivyo sisi nasi tunaweza na tunapaswa kuhudumu katika uweza wa Roho Mtakatifu
(Lk 4:18).

2. Yesu Alishinda Majaribu Ya Shetani

Kule nyikani Yesu alikuwa dhaifu na mwenye njaa wakati Shetani alipomjaribu ili atumie vibaya uweza wake kubadilisha mawe kuwa mkate. Tena Shetani alimjaribu  ili akwepe mateso ya Msalaba, na kisha tena akamjaribu ili ajikweze, lakini kila mara Yesu alimkatalia Shetani na akachagua kuwa mwaminifu kwa Mungu na kwa kusudi lake. Shetani aliondoka zake akiwa ameshindwa (Mk 1:13) (Mt 4:1-11).

3. Yesu Aliyapa Mahubiri Kipaumbele

  1. Alisema ujumbe wake ni habari njema.

  2. Alisema ufalme wa Mungu umekaribia.

  3. Alisema wakati umewadia.

  4. Aliwataka watu watubu na kuamini (Mk 1:14).

Mara kadhaa tunashuhudia habari za Yesu kimyakimya na kwa upendo kupitia maisha yetu, lakini hatimaye inabidi watu wapewe changamoto ya kutubu, wamgeukie Mungu na kutubu, au la. Asije mtu akasema kwamba kuhubiri si muhimu. Miguel Diez alikuwa na wasikilizaji 3,000 katika mkutano wa hadhara huko Ecuador, Pensacola. Kanisa huko Florida limeshuhudia waamini wapya 100,000 katika kipindi cha miaka miwili; na Carlos Anacondia wa Argentina ameshuhudia zaidi ya watu 8,000,000 wakimpokea Kristo kupitia mahubiri.

4. Yesu Aliujua Wakati Wa Mungu

Yesu alifanya kazi hadi alipofikia miaka thelathini lakini Herode alipomweka Yohana gerezani, hiyo ilikuwa ni ishara ya Mungu. Yesu alijua wakati wake umewadia. Tunaambiwa tukeshe, ili tupate kujua ni wakati gani Yesu yuko mlangoni. Kama tukiangalia kwa jicho moja neno la Mungu la unabii, na kanisa, na Israeli; na jicho lingine tukaangalia matukio ya ulimwengu, tutazijua nyakati (Mk 13:28-36) (Mt 16:1-3).

  1. Nuhu alizijua nyakati, akajenga safina.

  2. Musa alizijua nyakati, akaongoza watu wa Mungu kutoka utumwani.

  3. Danieli alizijua nyakati, akaomba ili kwamba watu wa Mungu waliopelekwa utumwani wapate kuachiliwa.

  4. Mungu aliujua wakati, akamtuma Yesu.

  5. Yesu aliujua wakati, akahubiri.

5. Yesu Aliwaita Wengine Ili Wamsaidie

Hakufanya kila kitu peke yake (Mk 1:16-20). Watu waliusikia mwito wa Kristo na kutii bila kukawia, wakaacha kila kitu na kumfuata Yesu, hivyo kwamba mashahidi waliongezeka na kushirikiana kufanya kazi iliyokuwa mbele yao.

  1. Kwanza alikuwako Yesu peke yake.

  2. Kisha, Yesu na wale Thenashara.

  3. Halafu, ikawa ni wale Thenashara na wengine 3,000 zaidi.

  4. Halafu 3,000 wakawa Wayahudi 5,000.

  5. Kisha watu kutoka mataifa mengine wakajiunga.

  6. Hatimaye Injili ikafika Afrika na Asia, na kuendelea.

6. Yesu Alidhihirisha Uweza Wa Mungu

Alimtoa pepo (Mk 1:25).
Aliponya mwenye homa (Mk 1:31).
Aliponya wengi na kutoa mapepo (Mk 1:33,39).
Alimponya mwenye ukoma (Mk 1:42).

Kila wakati Yesu alipoonesha uweza wa Mungu ambao ni upendo na huruma ya Mungu ikifanya kazi, habari zilienea (Mk 1:28,45), kiasi kwamba mji wote ulikuja kumwona (Mk 1:33,37).

7. Yesu Aliomba Kwa Dhati

Yesu alitenda kazi alizoona Baba yake akitenda (Yn 5:19), na ili aweze kutenda kazi hizo, alitenga muda wa kumsikiliza Baba yake. Wakati mwingine ilikuwa ni alfajiri au usiku wa manane au usiku mzima; akiwa faraghani au hadharani. Hatimaye alijua ni nini la kufanya
(Mk 1:35).

8. Yesu Alijitoa Kwa Watu

Alikuwa na fursa ya kukaa mahali pamoja na kujulikana, lakini Yesu alitaka kwenda hata vijiji vya jirani ili ahubiri huko pia (Mk 1:37-39). Yesu alipenda watu, hata wale wasiopendeka kama vile wenye mapepo wachafu, yule mwanamke mgonjwa, na wenye ukoma. Kwa Yesu lilikuwa ni suala la kujitoa ili kuwafikia watu wengi zaidi na upendo wa Mungu. Matokeo yake ni kwamba watu wengi walimjia kutoka kila mahali, na bado wanaendelea kumjia.

Yesu alikuwa ni mwanadamu katika uweza wa Roho Mtakatifu. Yesu akasema kwamba ye yote atakayemwamini atatenda si hayo tu, ila na yaliyo makubwa zaidi kwa uweza wa Roho Mtakatifu yuleyule ambaye Yesu alimtuma kwetu.

9. Maswali Ya Kujiuliza

  1. Je, una mipango gani ya kuwafikia watu?

  2. Je, unajitoaje kwa ajili ya maombi?

  3. Je, unatumia karama za Roho?

  4. Je, unaitikia wito wa Yesu?

  5. Je,waweza kuona kwamba wakati wa Mungu ni sasa?

  6. Je, kuhubiri umekupa umuhimu wa kwanza?

  7. Je, unashinda majaribu ya Shetani kila siku kwa maombi, kwa neno na kufanya maamuzi matakatifu?

  8. Je, ulimpokea Roho Mtakatifu siku ulipoamini, na je, unaendelea kujazwa Naye kila siku?



Kwa Kumalizia Omba Kwa Ajili Ya Watu Wa Ulimwengu
Huu Ambao Bado Hawajafikiwa Na Injili; Wataje Kwa Majina
 

Azerbaijan

Jina la Watu

Lugha Yao

Idadi Yao

Avar

Avar

46,000

Tat, Mussulman

Tat, Mussulman

22,000

Tatar

Tatar

29,000

Turk

Turkish

19,000

 


 1985 - 2007

With many thanks to Pastor Dastan Mboera, Dar es Salaaam, Tanzania
for this revision and translation from the original English
mboeradsk @ yahoo.com


© Dr Les Norman  The DCI Trust, UK
Permission is granted to provide copies at cost price for study purposes
but not for sale or commercial purposes. Freely you have received, so please freely give.

Support Pages   Index To All Lessons   School of Finances  

World Christian News   
Who Are We?   Site Index